MKUU WA WILAYA IRAMBA AZINDUA ZAHANATI YA KIJIJI CHA NDURUMO


Wananchi wakimbeba kwa furaha Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman, Mwenda,   baada ya kuzindua  Zahanati katika Kijiji cha Ndurumo, Kata ya Kidaru mkoani Singida. (Picha na Hemedi Munga).


Na HEMEDI MUNGA

Juhudi za wananchi wa Kijiji cha Ndurumo Kata ya Kidaru wilayani Iramba mkoani Singida zimewaibua viongozi kumalisha ujenzi wa zahanati kwa lengo la kufikisha huduma za afya karibu na wananchi.

Halmashauri ya wilaya hiyo imetoa takribani sh milioni 79 ambazo zimekamilisha ujenzi wa Zahanati ambayo ameizindua Mkuu wa wilaya hiyo, Suleiman Mwenda.

Akizungumza katika hafla hiyo baada ya uzinduzi wa Zahanati hiyo katika kijiji hicho, Mwenda ameupongeza uongozi wao na Mwenytekiti wa Halmashauri hiyo, Innocent Msengi kwa kukamilisha Zahanati 10 na usimamiaji madhubuti wa miradi ya maendeleo.

Pia, amempongeza Mbunge wa jimbo hilo, Waziri wa Fedha,  Dk. Mwigulu Nchemba kwa kuhakikisha  anawasemea watu wake bungeni na kufanikisha kupata fedha za  kujenga vituo vya afya sita ndani ya miaka mitatu ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

"Ndugu zangu hakika Rais Dk. Samia ametekeleza wajibu wake kwa kuboresha huduma za afya," amesema.

Aidha, amesema kwa upande wa sekta ya  nishati ya umeme  Rais Dk. Samia amehakikisha umeme unafika katika kila kijiji huku akiahidi kufikisha katika kila kitongoji.

" Baada ya miezi miwili umeme utafika hapa na katika kila kitongoji kati ya vitongoji 393 vya wilaya hiyo vyote vitapata umeme," amesema Mwenda.

Amesema Rais Dk. Samia ameleta takribani sh milioni 800 kwa lengo la kununua vifaa tiba na leo mmeona vifaa pea tatu tatu zipo katika zahanati hii.

Pia, barabara  mpango wa serikali ni kujenga barabara ya kutoka Shelui hadi Sibiti na barabara ya kutoka Kizaga hadi Singida mjini kwa kiwango cha lami.

" Huyo ndio  Rais Dk. Samia  anayafanya makubwa kwa wananchi wake," amesisitiza.

Mwenda ameomba namna  pekee ya kumlipa rais huyo  ni kumpa kura za kishindo kwa lengo la kuendelea kupata huduma hizo karibu na kwa wakati.

Pia, amewaasa wananchi hao na viongozi wa Kimila  kuwapa ulinzi wa siri na dhahiri huku akionya  kutosikia watumishi hao wanalala ndani wanajikuta wako nje.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Msengi amesema hitajio la jamii liliwasukuma wao kutoa fedha kukamilisha ujenzi huo.

" Bila kusita kwa sababu nilifia mwenyewe na kuona nguvu ya jamii, umuhimu wa jambo hili nilishawishi kupata sh milioni 79 za ujenzi huu," amesema.

Akizungumza katika sherehe hiyo, Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Philipo Manguli amemuomba Mkuu wa Wilaya kuwafikishia salamu kwa Rais Dk. Samia kwa kuwapa fedha za  kukamilisha bweni zaidi ya  sh milioni 80, fedha za kujenga madarasa zaidi ya sh milioni 100, kujenga jengo la kujifungulia sh milioni 90,  sh milioni  250 kujenga  nyumba za walimu na matundu ya vyoo katika kijiji cha Mwamapuli.

"Hizi ni fedha za Dk. Samia na tutamuonesha upendo wetu kwenye sanduku la kupiga kura, 2025," amesema.

Ameongeza kuwa Dk. Samia amejiatahidi kufungua uchumi na kufanikisha wao kupata fedha nyingi zinazosaidia kutatua kero za wananchi kwa wakati.

"Tunamuhakikishia rais wetu 2025 kura zote zakwake aendelea kututumikia tupate  maendeleo," amesisitiza.

Naye Mzee wa Jadi,  Chandika Halawa, Amewaomba wananchi kuheshimu Chama Cha  Mapinduzi (CCM) na serikali kwa sababu ni mfano wa  baba na mama kuwajali wananchi wake.

Amesema haijawi kutokea tangu mwaka 1973 alipozaliwa kijiji hicho kupata huduma hiyo.


Mkuu wa wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda, akizungumza na wananchi namna Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anavyowajali kwa kuwaletea fedha za kujenga miradi ya maendeleo, wakati wa uzinduzi wa Zahanati ya Kijiji cha Ndurumo, Kata ya Kidaru, mkoani Singida.


Zahanati ya Kijiji cha Ndurumo Kata ya Kidaru wilayani Iramba mkoani Singida, iliyozinduliwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Mwenda.