UWT TEMEKE WAPOKEA UTEKELEZAJI ILANI KWA MADIWANI VITI MAALUMU

Na Mwandishi Wetu

 Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Temeke,  umepokea taarifa  za madiwani wa viti maalumu  kuhusu utekelezaji wa  Ilani ya CCM  kwa kipindi cha miezi sita  iliyopita  na kuahidi kuendelea kuwasimamia kikamilifu madiwani hao kutimiza wajibu wao.

Akizungumza wakati wa Baraza la UWT Temeke,  Mwenyekiti wa  umoja huo wilayani humo, Lawama  Mikidafi, amesema baraza litaendelea kufuatilia utekelezaji wa Ilani  ya CCM na miradi inayotekelezwa wilayani humo.

“Sisi UWT tumejipanga vizuri kuhakikisha kila shughuli inayofanywa na madiwani hawa tunaipata kupitia utekelezaji. Sisi tutazifanyia tathimini na tunamipangokazi tuliyoweka ambayo tunataka ifikiwe,”amesema Lawama.

Akifungua mkutano wa Baraza, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Abass Mtemvu, ameitaka UWT  kuimarisha umoja na kuondoa tofauti zao katika kutumikia wananchi ambao wanamatumaini makubwa na Chama.

“Pendaneni na muwe wamoja  yaani mtafanya kazi kubwa Temeke. Temeke  mnauwezo mkubwa na  mnarasilimali nyingi  lakini mnashindwa kusaidia kina mama,”amesema Mtemvu.

 Mtemvu amesema hata   mikopo inayotolewa  na halmashauri kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu wanaonufaika nayo siyo  wanawake  CCM. 

“Kwa sababu hamuelewani. Hebu wapeni uwezo wanawake hawa  kwa sababu siasa ni uchumi.  Wafanyeni kina mama wawe na uwezo  mtafika mbali,”ameeleza Mtemvu.

 Mjumbe wa Halmashauri Kuu  Taifa (NEC) ya CCM,  Juma Simba ‘Gadaffi’, amesema  kutokana na hali inayoendelea  ndani ya UWT Temeke  lazima kuna sababu zilizo jificha.

“ Tutakaa na UWT, Kamati ya  Utekelezaji ya Wilaya. Hapa kuna jambo na hilo jambo  inawezekana  nongwa za uchaguzi hazijaisha  ndani ya UWT, ndani ya Chama  wilaya au mkoa,”amesema Simba. 

Baadhi ya madiwani wa  viti maalumu  wilayani humo wamempongeza Mwenyekiti  wa CCM, Rais Dk. Samia kwa utekelezaji wa miradi  ya maendeleo wilayani humo na kwamba  wamejipanga kikamilifu  kuhakikisha Chama kinaibuka na ushindi mkubwa katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mapema mwakani na Uchaguzi Mkuu wa  Mwaka 2025.