ROBERTINHO AWATAKA WACHEZAJI KUPOTEZEA FURAHA YA UBINGWA NGAO YA JAMII, WAGEUKIE LIGI KUU

Na Mwandishi Wetu

Kocha wa Simba, Roberto Oliviera 'Robertinho' amewataka wachezaji wake kupotezea furaha za ubingwa wa Ngao ya Jamii na kugeukia Ligi Kuu.

Ligi Kuu Tanzania Bara imeanza kutimua vumbi leo ambapo timu sita zilishuka dimbani huku Simba ikitarajiwa kuanzia ugenini keshoketwa dhidi ya Mtibwa Sugar.

Simba ilitwaa ngao hiyo, Jumapili iliyopita, baada ya kushinda penalti 3-1 baada ya kumaliza dakika 90 bila kufungana, katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi akiwa mjini Morogoro, Robartinho amesema wanapaswa kusahau furaha za ubingwa na kuanza upya.

Amesema hawana muda wa kupoteza na wanatakiwa kuwa makini kwa kuanzia mchezo wa kesho kupambana kuhakikisha wanapata matokeo mazuri iwe wanacheza ugenini au nyumbani.