Na HEMEDI MUNGA, Iramba
Mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Godfrey Mnzava amewapongeza wananchi wanaoongozwa na Mkuu wa wilaya ya Iramba Mkoani Singida, Suleiman Mwenda kwa kutafsiri falsafa ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuhusu kuweka mazingira rafiki ya biashara na uwekezaji.
Pongezi hizo, amezitoa leo baada ya kuweka jiwe la Msingi katika Kiwanda cha Kukamua Mafuta ya Alizeti (Singida Adim Oil Mills) kilichopo kata ya Kyengege wilayani hapa.
"Mmeweka mazingira rafiki, hivyo mwenzetu huyu Hamoud Adim ameona eneo pekee na salama la kuweka mtaji wake ni hapa Iramba."
Mbio za Mwenge wa Uhuru zimefanikwa kutembelea, kuona, kuweka mawe ya msingi, kupata taarifa mbalimbali ikiwemo kuizindua miradi saba yenye thamani ya sh bilioni 5.084 ambazo zilitolewa na serikali anayoiongoza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.