SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC), limesema hawatapandisha nauli kwa abiria wasafiri wakati wa kipindi hichi cha Sikukuu za mwisho mwaka.
Kuhusu Mabehewa mapya 21 yanayokwenda mkoani Kigoma, Kadogosa amesema mabehewa hayo yamefanyiwa kwa mujibu wa sheria na baada ya kupitishwa na Mamlaka ya Usafiri Ardhini (LATRA), yamekidhi mahitaji ya kusafirisha abiria.
“ Hatimaye leo tumeanza safari rasmi kwa kutumia mabehewa mapya 21 ya Meter Gauge (MGR) kwenda Kigoma na treni itakaporejea Dar es Salaam, itaanza safari ya kwenda Kilimanjaro ambapo mabehewa hayo yatasaidia kupunguza msongamano wa abiria kugombania upatikanaji wa tiketi,” amesema.
Kadogosa amesema mabehewa hayo yalinunuliwa na serikali kwa lengo la kuongeza ufanisi katika kutoa huduma ya usafiri wa reli nchini.
Aidha Kadogosa amesema safari rasmi zimeanza baada ya majaribio ya awali umbali wa kilometa 400 kutoka Dar es Salaam –Morogoro ambapo LATRA imeridhia mabehewa hayo kuanza kazi rasmi.
Mabehewa mapya ya abiria ni 20 ambayo yamebeba jumla ya abiria 1500 wanaotoka Dar es Salaam kwenda Kigoma huku behewa moja likitengwa kwa ajili ya huduma za mgahawa.
“Kufuatia ununuzi wa mabehewa hayo, Shirika hilo limeongeza idadi ya mabehewa ya treni ya Deluxe kwenda mikoa ya Kaskazini kutoka mabehewa sita hadi 16 na njia ya reli ya kati kutoka mabehewa 4 hadi 20,” alifafanua.
Alisema TRC itaongeza idadi ya mabehewa kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu watakaojitokeza kutumia usafiri huo.
Akizungumza na Blog hii mmoja kati ya abiria waliosafiri na treni hiyo, aliyejitambulisha kwa jina la Sheha Ibrahim, amesema kuwa mabehewa hayo yako vizuri na yakiendelea hivyo yatavutia watu wengi kutumia usafiri wa treni na kuachana na mabasi.
‘’Nauli ya usafiri huo haijaongezwa kwani wanatumia za zamani za treni ya deluxe ambayo kwa daraja la kulala ilikuwa sh. 65,000 kutoka Dar es Salaam- Kigoma.
‘’ Ni ukombozi kwetu Watanzania kupata mabehewa kama haya kwa sababu yaliyokuwepo hayana hali nzuri hivyo itatusaidia sisi kuachana na mabasi,” amesema.
Abiria wakipanda treni ya kwenda Kigoma, katika kituo cha Kamata, Dar es Salaam, ambapo wamesafiri kwa kutumia mabehewa mapya ya Shirika la Reli (TRC), yaliyowasili hivi karibuni.