SPIKA DKT. TULIA AWATAKA MAJAJI KUTENDA HAKI






Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, amewataka Majaji wa Mahakama nchini kuzingatia weledi, kufuata misingi ya kisheria na kutenda haki katika kazi zao.

Dkt. Tulia ameyasema hayo, wakati akifungua  Mkutano wa Chama cha Majaji Wanawake Tanzania (TAWJA) uliofanyika mkoani Tanga,  kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa ni muhimu kuelewa kuwa siku zote mafanikio yao yasipimwe kwenye hukumu na maamuzi mangapi yaliyoandikwa na kutolewa tu, idadi ya vikao vya kesi walivyohudhuria au idadi ya mizozo iliyomalizika bali ni kwa jinsi gani nafasi zao katika Mahakama na maamuzi yametoa tafsiri katika kuiwezesha jamii kuondokana na ubaguzi na ukatili dhidi ya wanawake.

“Ni wakati wa kusimama imara kuweza kutimiza majukumu yenu hata pale kwenye vikwazo na changamoto za kijamii, kiimani na kitamaduni. Tukifanya hivyo, bila shaka tutakuwa sehemu ya kumwaga tone la maji litakalosambaa na kuwa dimbwi baadaye mto, ziwa na kuenea katika bahari kubwa ya jamii, na hivyo kufanya mwanamke kutoonekana Mhanga bali kuonekana Shupavu, Mpambanaji na Kiongozi.” Amesisitiza Dkt. Tulia

Sambamba na hayo, Mhe. Spika amesema kuwa Bunge lake lipo tayari kupokea maoni ya mabadiliko ya sheria zilizopitwa na wakati ili kuzifanyia maboresho kwa lengo la kuhakikisha haki za makundi mbalimbali katika Jamii zinalindwa.