MTWARA YAJIVUNIA MASHINDANO YA MAJESHI

Kamishna wa Uhamiaji Huduma za Sheria, Novaita Mroso, akimkabidhi Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dk. Anna Makakala, kombe la Ubingwa  wa soka wa mashindano ya Majeshi yaliyomalizika hivi karibuni, mkoani Mtwara.

 

NA MWANDISHI WETU

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Ahmed Abbas, amesema mashindano ya majeshi ambayo yalikuwa yanafanyika yameongeza kipato katika mkoa wake.

Mashindano hayo ambayo yaliandaliwa na Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA), yalifanyika kwa siku 14 katika viwanja vya Chuo cha Ufundi na Nangwanda.

Timu zilizokuwa zinashiriki mashindano hayo ni Uhamiaji, SMZ, Magereza, Polisi, JKT, Ngome na Zimamoto zikicheza michezo ya riadha, mpira wa miguu, mpira wa kikapu, mpira wa mikono, mpira wa wavu, netiboli, ngumi, judo na kurusha shabaha.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Kanali Abbas, kulikuwa na idadi ya watu wasiopungua 5000 waliokuwa wanashiriki mashindano haya.

“Watu wamekula, wamekunywa na kulala hii kwetu imeongeza pato la mkoa naamini hata wafanyabiashara walikuwa na furaha wakati mwingi,” amesema. 

Alisema mashindano hayo pia yameongeza uhusiano mzuri kati ya vyombo vya ulinzi na wakazi wa mkoa huo kutokana na kuwa nao kwa karibu.

“Jeshi na wananchini ni watu tunaoshirikiana vizuri, kama mlivyoona wamejitokeza kuchangia damu ambazo zitawasaidia wagonjwa wa mkoa wangu hii kwetu ni kubwa sana,”amesema.

Mashindano yalianza kutimua vumbi Februari 9 hadi Februali 21na yalifungwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Jumanne Sagini.