WAKANDARASI WANAOTEKELZA MIRADI YA MAJI KAMILISHENI KWA WAKATI NA VIWANGO-DC LUDEWA




Na Hemed Munga, Ludewa


Wakandarasi  wanaotekeleza miradi ya maendeleo, ikiwemo sekta ya maji wametakiwa kufanya kazi kwa ufanisi, ubora, kukamilisha kwa wakati na   kuzingatia thamani ya fedha.


Wito huo, umetolewa na Mkuu wa  Wilaya ya  Ludewa, mkoani Njombe,Victoria Mwanziva, alipofanya ziara ya kimkakati ya kukagua wa miradi ya maji wilayani humo, mkoani Njombe.


Amesema kupitia mradi huo utakapokamilika, wananchi watapata huduma ya majisafi na salama yatakayowatosheleza katika matumizi yao.


Victoria amesema kazi kubwa inayofanywa na  Rais Dk.  Samia Suluhu Hassan katika sekta ya maji wilayani humo, kuhakikisha wananchi wanapata huduma maji ya uhakika kwa lengo la kumtua mama ndoo kichwani.


"Ndugu zangu wananchi hakika tunamshukuru Rais Dk. Samia kwa sababu ametuletea Wanaludewa fedha Sh. bilioni 13.866, ambazo zimetekeleza  miradi saba ya maji ambayo itaongeza huduma ya upatikanaji maji kutoka asilimia  74.3 hadi  79.7, vijijini na asilimia 100 kwa wakazi wa mji wa Ludewa", amesema.


Pia,  Victoria amewataka wataalamu wa ngazi zote kuendelea kuielimisha jamii kutunza vyanzo vya maji na miundombinu kwa lengo la kunufaisha vizazi vijavyo. 


Victoria ameongozana na viongozi mbalimbali wilayani humo, katika ziara hiyo Kata ya  Mavanga, Ludewa, Iwela, na Manda  kukagua hali ya upatikanaji wa maji na hali za miradi inayotekelezwa.