WASHAURIWA KUMUUNGA MKONO RAIS DK. SAMIA KWA KUANZISHA SACCOS KUEPUKA MIKOPO KAUSHA DAMU

DIWANI wa Viti Maalumu na Mlezi wa  Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Kata ya Bunju, Grace Mwashala (kushoto) akimkabidhi   Mwenyekiti wa Umoja huo wa kata hiyo, Mercy Semgori (kulia)  msaada wa  vitenge, kadi  za umoja huo, fedha taslimu  na  reja kwa lengo za kuanzisha mradi ,wilayani Kinondoni, Dar es Salaam . Katikati (mwenye kiremba chekundu) ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi,  Fatuma Kange. (Na Mpigapicha Wetu).




NA MWANDISHI WETU, DAR


Wanawake nchini wameshauriwa kuanzisha vikundi vya kuweka na kukopa (SACCOS) kuepuka mikopo  yenye riba kubwa  ikiwemo ya kausha damu.

Pia, wametakiwa kuanzisha  vikundi vya miradi  ya ujasiriamali na kuungishana kwa kununua bidhaa wanazo zalisha hali itakayo wainua kiuchumi.

 

Wito huo umetolewa na Mlezi wa Kata za Bunju na  Makongo , wilayani Kinondoni,  Diwani wa Viti Maalumu, Grace  Mwashala, alipokuwa akikabidhi misaada kwa  Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Kata ya Bunju, Dar  es Salaam.


Diwani huyo amekabidhi  vitenge, fedha taslimu , kadi za UWT na reja ambazo  wanachama wa UWT  Bunju watavutimia kuanzisha mradi .


Amesema vitenge hivyo ni kwaajili ya kukopeshana kisha fedha kuingizwa katika mfuko maalumu wa UWT  wa Kata  ambapo alitoa kiasi cha sh. 20,000 kufungua akaunti maalumu ya benki kwaajili ya miradi.


Grace amesema, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amekuwa  mstari wa mbele kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kiuchumi, hivyo ni muhimu kumuunga mkono kwa kuanzisha vikundi vya ujasiriamali na SACCOS.


“Anzisheni  SACCOS ziwasaidie  kujikwamua kiuchumi. Mnaweza wanawake. Acheni mikopo hii ya kausha damuna inayotoza riba kubwa,”ameeleza  Diwani Grace.


Mwenyekiti wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi, Fatuma Kange, alieleza umuhimu wa wanawake kuwa na SACOSS, zitakazo waepusha na mikopo yenye riba kubwa ya benki na kausha damu.


Kange ameeleza kuwa jicho la Rais Dk. Samia ni kuona wanawake wanainuka kiuchumi na ndiyo maana alianzisha Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalumu ili kumwezesha  mwanamke.


Aidha Kange, amewaasa wanawake kuungishana katika bidhaa wanazotengeneza na kuhakikisha zinakuwa na msimbo milia 'Bar Code' ili  zikidhi  viwango.