Watumishi watakiwa kujiandaa kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa

IGUNGA - TABORA

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Igunga mkoani Tabora, Selwa Abdalla Hamid ametoa wito kwa watumishi kujiandaa kimwili na kiakili kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa ambao unatarajiwa kufanyika ifikapo mwezi Novemba 27, 2024.

Selwa ametoa wito huo wakati wa semina fupi ya Mwalimu Spesho Umetufunza Tumekutunza iliyofanyika katika ukumbi wa Sakao wilayani hapa ambayo  iliendeshwa na Benki ya NMB kwa lengo la kujengeana uwezo kuhusu maboresho yaliofanywa na benki hiyo ikiwemo kuomba mkopo kupitia mfumo wa kiutumishi ulioanzishwa na serikali.

"Ndugu zangu sisi wenyewe tukiwa ni watumishi tunahaki na wajibu wa kushiriki katika uchaguzi, hivyo niwaombe maandalizi yetu yaanze sasa," amesema na kuongeza kuwa:

"Ni jambo la msingi kushirikiana katika uchaguzi huu, hivyo twende tukahamasishane kujiandikisha na kupiga kura muda utakapofika."